JIFUNZE IBADA YA FUNGA, NGUZO ZA FUNG, SUNNAH ZA FUNGA, FADHILA ZA FUNGA NA YANAYOHARIBU FUNGA.

JIFUNZE IBADA YA FUNGA, NGUZO ZA FUNG, SUNNAH ZA FUNGA, FADHILA ZA FUNGA NA YANAYOHARIBU FUNGA.

Darsa za Funga

Ustadh Rajabu

DARSA ZA FUNGA

DARSA ZA FUNGA. Maana.
Maana ya funga kisheria ni kujizuia na vyenye kufunguza toka kuchomoza kwa alfajiri mpaka kuzama kwa jua pamoja na kuwa na niya ya kufanya ibada kwa ajili ya Allah.


Fadhila za funga
Amesema mtume (s.a.w) kuwa Allah (s.w) amesema: kila amali ya mwanaadamu ni kwa ajili yake isipokuwa funga. Kwa hakika hiyo funga ni yangu, na mimi ndiye ninayeilipa ( thawabu) na funga ni ngome. Basi atakapfunga mmoja wenu asizungumze maneno ya upuuzi, wala asifanye mambo machafu na ya kijinga. Basi ikitikea mtu amemtukana au kumpiga yeye (asilipize) bali amwambie 'nini mimefunga'.


Na akasema Mtume (s.a.w) 'na ninaapa kwa yule ambaye nafsi ya Muhammad ipo kwenye mkono wak: hakika harufu ya mdomo wa mwenye kufunga inapendeza zaidi mbele ya Allah siku ya kiyama kuliko harufu ya mafuta ya misk. Na ana mwenye kufunga furaha mbili: atakapofutari na atakapokutana na Mo;a wake atafurahia funga yake. (Bukhari na Muslim)


Amesema Mtume kuwa Mwenye kufunga ramadhani akiwa na imani na na kutarajia malipo kwa Allah, atasamehewa madhambi yake yaliyotangulia.(Bukhari na Muslim)


Amesema Mtume kuwa: hakika kuna peponi mtango unaitwa BABU RAYAAN watauingia mlango huo wenye kufunga siku ya kiyama. Na hatauingia mlango huo yeyote isipokuwa watu hao tu na itasemwa 'waku wapi wenye kufunga' basi hapo watasimama na hataingia yeyote isipokuwa wao, na pindi watakapoingia utafungwa na katu hataingia yeyote. (Bukhari na Muslim)


Mgawnyiko wa funga.
Basi jua ewe ndugu kuwa funga zimegawanyika katika makundi makuu mawili nayo ni :
1.funga za wajibu (lazima)
2.Funga za sunnah (zisizo za lazima)


1.funga za wajibu
Hugawanyika funga hizi katika makundi makuu matatu ambayo ni:
1.funga ambazo ni wajibu kwa kuingia wakati maalum. Nayo ni funga ya ramadhani
2.Funga amabzo ni wajibu kutokana na 'ila nayo funga za kafara
3.Zilizo wajibu kwa kujiwajibishia mtu mwenyewe. Nazo ni funga za nadhir


FUNGA YA RAMADHAN
Ni wajibu kwa kila `muislamu aliye balehe na kuwa na akili timamu, na awe mkazi wa mji (asiwe msafiri). Funga pia ni nguzo katika uislamu. Na funga ya ramadhani imethibiti katika qurani na katika sunnah. Amesema Allah: enyi mlioamini kumefaradhishwa kwenu kufunga.'..'


Amesema Mtume kuwa: umejengwa uislamu juu ya nguzo tano: kutoa shahada kuwa hakuna Mola apasaye kuabudiwa ila Allah na kuwa Muhammad ni mtume wake, na kusimamisha swala, na kutoa zaka na kuhiji na kufunga mwezi wa ramadhani. (Bukhari na Muslim)


Fadhila za funga ya ramadhani
Amesema Mtume: utakapoingia mwezi wa ramadhani, hufunguliwa milango ya peponi na hufungwa milango ya motoni, na hufungwa minyororo shetani. (Bukhari na Mslim)


Amesema Mtume: mwenye kufunga ramadhani akiwa na imani na kutarajia malipo kwa Allah atasamehewa madhambi yake yakiyotangulia. (Bukhari na Muslim)


Amesema Mtume: swala tano, na swala ya ijumaa mpaka ijumaa, na funga ya ramadhani hufuta madhambi mpaka ramadhani yaliyopo kati yao, pindi kukiwepo na kujiepusha na mashambi makubwa. (Bukhari na Ibn Maajah)


Kuna katika mwisho wa mwezi huu usiku wa laylat-alqdir, usiku ulio bora kuliko mieze elfu moja. Amesema Allah '.(usiku wa )laylatul-qadir ni mbora kuliko mieze elfu moja'. (suratul-qadir)


Kuthibiti kwa mwezi
Ni wajibu kufunga kwa kuthibiti kwa mwezi. Na huku hunatokea kwa namna mbili
1.kuonekana kwa mwezi wa ramadhani (mwezi mwandamo)
Amesema Allah(s.w): Mwenye kushuhudia mwezi (mwandamo) basi na afunge.'.'
Na amesema Mtume (s.a.w) pindi mtakapouona fungeni na mtakapouona fungueni...:(Bukhari). Pia amesema Mtume: '..utakapozibwa (na mawingu mkawa hamuuone) timizeni siku thelathini (Bukhari)


2.kupata taarifa juu ya kuonekana kwa mwezi
Hapa kinachozungumziwa ni pale mwezi ukawa umeonekana na wachache katika watu na zikatumika taarifa zile kuwajulisha ambao hawakuuona. Jambo hili klinajuzu. Na hapa ndipo zinapatikana mas-ala za ikhtilafu juu ya kuonekana kwa mwezi. Na tutazungumzia kipengele hiki zaidi kwenye darsa za mbele.


Sharti za kusihi kwa funga
1.Kuwa twahara kuepukana na hedhi na nifas. Ni hii nisharti ya kusihi kufunga na pia ni wakati wa kulipa


2.Niya:niya ni sharti katika kuswihi kwa funga, Amesema Mtume: hakika amali yoyote hulipwa kwa kuzingatia niya...' (Bukhari na Muslim). Na maulamaa huzungumza kuwa niya ni lazima ibainishwe kuwa ni ya kufunga ramadhani na iwe kabla ya alfajiri. Na inapasa kutia niya kila siku usiku


Nguzo za funga
1.kujizuia kutokana na vyenye kufunguza toka kuchomoza kwa alfajiri mpaka kuzama kwa jua. Kma kula, kunywa, kuingiliana kimwili, kijitapisha, kujistarehesha kwa mkono (punyeto) n.k


Sunnah za funga
1.kula daku.
Amesema Mtume: kuleni daku kwa hakika mna baraka katika kula daku (Bukhari na Muslim). Na kula daku sio lazima kukusanya mavyakula mengi na mazuri hapana, Mtume (s.a.w) amesema: fanyeni daku japo kwa maji (Ibn Majah). Na bora ya daku ni kula tende kama alivyosema mtume katika hadithi aliyoipokea Abuu Daud nayo ni hadithi sahihi.


2.kuchelewa katika kula daku.
Ni sunnah kuchelewa kula daku mpaka karibia na adhana ya alfajiri. Amesimulia Zaid Ibn Thabit kuwa tulikuwa tukila daku pamoja na mtume kisha kasimama kuiendea swala, akauliza Anas Ibn Malik kumuuliza Zaid: kulikuwa na urefu wa muda gani kati ya muda wa daku na adhana ya swala akasema Zaid: ni kiasi cha kumaliza kusoma aya 50 (za quran) (Bukhari na Muslim). Wakati huu kulikuwa na Adhana mbili katika swala ya lfajiri hivyo Mtume akawaambia Masahaba: atakapoadhini Ummul-maktum kuleni na kunyweni na atakapoadhini bilali msile wala msinywe.(Nisai).


3.Kuwahi kufuturu.
Amesema Mtume: watu hawaachi kuwa wapo kwenye here maadamu wanawahi kufuturu. (Bukhari na Muslim). Yaani ni heri tupu inapatikana kwa kuwahi kuftari. 4.Kufuturu kwa kitu cha majimaji au kwa tende.amesimulia Anas kuwa alikuwa mtume anafuturu kwa kitu cha majimaji kabla ya kuswali na akikosa chenye majimaji basi hufuturu kwa tende na akikosa hufuturu kwa maji. (Abu Daud na tirmidh)


5.Kuomba dua wakati wa kuftari. Alikuwa Mtume akiomba dua hii 'dhahaba dhw-dhwamau, wab-taliyatl-'uruuq wathabatil-ajru in shaa Allahu (Nisai)


6.Kujipinda katika kheri mbalimbali pamoja na kusoma qurani kwa wingi. Alikuwa Mtume anakundishwa qurani katika mwezi wa ramadhani


7.Kuacha maneno ya upuuzi,uongo na matendo machafu. Amesema Mtume mtu ambaye hawezi kuacha kuzungumza uongo na kufanyia kazi matendo ya uongo Allah hana haja na (funga yake mtu huyu.) kuacha chakula chake na kinywaji chake.(Bukhari) Na katika maneno mengine mtume anakataza kwa mwenye kufunga kufanya uovu na uchafu mwingine.


Mambo yenye kufunguza Swaumu:
Huharibika funga kwa kuvunja nguzo ya funga pamoja na sharti zake. Haya yenye kubatilisha funga yamegawanyika katika makundi makuu mawili nayo ni:-


1.yenye kubatilisha funga na kulazimika kulipa nayo ni;-
A)kula na kunya kwa makusudi. Mtu aliyekula au kunywa kwa kusahau funga yake haita haribika. Amesema Mtume (s.a.w): mwenye kusahau na hali ya kuwa amefunga, na akala na kunywa na aendelee na funga yake kwani hakika Allah amemlisha. (Bukhari na Muslim). Mwenye kula au kunywa kwa makusudi atakujalipa funga hii.


B)Kujitapishwa kwa makusudi. Amesema Mtume (s.a.w): mwenye kutapika hana haja ya kulipa funga ila mwenye kujitapisha kwa makusudi na alipe funga.(Tirmidh)


C)Kupatwa na hedhi
D)Kupatwa na nifasi
E)Kujistarehesha kwa mkono (punyeto)
F)Kukusudia kuvuja funga yaani kukusudia kuftari.
G)Kutoka kwenye uislamu.


2.yenye kubatilisha funga na kulazimika kulipa pamoja na kutoa kafara
Na hapa ni jambo moja tu nalo ni kufanya jimai. Amesimulia Abuu hurairah kuwa wakati tulipokuwa tumekaa na Mtume (s.a.w) ghafla akaja Mtu mmoja na akamwambia Mtume (s.a.w) ewe mtume nimeangamia Mtume akamuuliza una nini akajibu:nimefanya jimai na mke wangu na hali ya kuwa nimefunga. Mtume akamwambia je unae Mtumwa umuache huru, akasema sina, akamwambia:je unaweza kufunga kwa muda wa miezi miwili mfululizi? Akasema: siwezi. Akamwambia je unaweza kulisha masikini sitini? Akasema siwezi, basi pale Mtume akanyamaza. Akasema Abuu hurairah wakati tukiwa katika hali ile kukaletwa kwa mtume tende basi mtume akauliza yupo wapi aliyeuliza? Akasema nipo hapa, akamwambia chukuwa hizi tende ukatoe sadaka.'.'


Hivyo kafara ya mwenye kufanya jimai ni kuacha huru mtumwa au kufunga miezi miwili mfululizo au kulisha masikini sitini. Na hukumu hii pia ni sawa na mwanamke.


Mambo haya hayafunguulishi
1.kufunga mtu akiwa na janaba. Mtu aliyeamka na janaba anaruhusiwa kufunga katika mapokezi sahihi ni kuwa alikuwa Mtume (s.a.w) anaamka alfajiri akiwa na janaba anaoga kisha anaswali. (Bukhari na Muslim)


2.Kumbusu mke au kuchezeana bila ya kuingiliana, kwa mwenyekuweza kudhibiti matamanio yake. Ameseimulia Mama wa waumini Aisha kuwa alikuwa Mtume akinibusu akiwa amefunga na mimi nimefunga. Na katika mapokezi amesema 'alikuwa akinibusu na kunichezea akiwa amefunga.'..' (Bukhari na Muslim)


3.Kuoga au kujimwaga maji kichwani. Alikuwa Mtume akioga na wakati mwingine akijimwagia maji kichwani kutokana na joto au kiu kikali. (Abu dawd).


4.Kusukutua na kupandisha maji puani. Hili ni jambo linalojuzu na mtume ameruhusu ila akaweka tahadhari wakati wa kubalighisha maji yaani kuyapandisha maji kooni.


5.Kuonja chakula bila ya kukila amesema Ibn 'Abas kuwa: hakuna ubaya katika kuonja siki au chochote maadamu hakifiki tumboni


6.Hijama, kuchoma sindano au kutiwa madirip.


7.Kujipamba kwa wanja, mafuta n.k


8.Kupiga mswaki.


9.Mabaki ya chakula kwenye mdomo.


Walioruhusiwa kufungua mwezi wa ramadhani
Hawa wamegawanyika katika makundi matatu
1.kuna ambao inajuzu kufungua na kufunga
2.Ni wajibu kufungua
3.Haijuzu kwao kufungua.


1.wanaojuziwa kufunga au kufungua 1.mgonjwa. Watu wagonjwa inafaa kwao kufunga au kutofunga. Maradhi yapo katika namna tatu.


A)maradhi hafifu kama mafua ambayo hata hayaathiri funga hata kidogo. Ni haramu futofunga kwa maradhi ya namna hii.


B)Maradhi ambayo sio mkubwa lakini yanaathiri funga, hapa mgonjwa ana hiyari ya kufunga au kutofunga.


C)Maradhi makubwa ambayo mtu akifunga yatapelekea kuzidi kwa ugonjwa na hatimaye kudhoofu afya. Ni haramu kufunga kwa maradhi haya maana Allah amekataza kujiingiza kwenye maangamizo. Amesema Allah: 'na msiziue nafsi zenu' (quran 4:29)


2.msafiri: msafiri mwenye kusafiri safari ambayo inajuzu kupunguza swala inafaa kufungua. Na kama aatfunga pia funga yake inafaha. Ama kuhusu kipi kilicho bora kati ya kufunga na kutofungwa, maulamaa wameigawa safari katika makundi yafuatayo:


A)safari ambayo inatia uzito na mashaka kufunga. Hapa ni bora zaidi kutofunga kuliko kufunga. Imepokewa hadithi kutoka kwa Jabir kuwa alikuwa mtume katika safari, akaona kuna watu wapo katika hali flani akauliza wana nini hawa akajibiwa wamefunga na hapo akasema 'si katika jambo jema kufunga kwenye safari' (Bukhari). Pia katika safi nyingine watu walipokuwa wapo kwenye jua kali safarini mtume alisema: wameondoka watu waliofungua leo na malipo ' (Muslim)


B)Safari ambayo haina shaka wala taabu katika funga. Hapa maulamaa wamesema katika hali hii kufunga ni bora zaidi, kwa kauli ya Allah: aliposema 'na mkifunga ni bora kwenu'(quran 2:184)


C)Ikiwa safari inamashaka makubwa na taabu kiasi kwamba inaweza kusababisha taabu na maangamivu. Hapa kutofunga ni jambo la lazima, yaani ni haramu kwa msafiri kufunga.


Muda wa kufungua.
Maulamaa wamnaeleza kuhusu ni muda gani mtu anatakiwa afungue katika hali zifuatazo:-


1.Kuanza safari kabla ya alfajiri. Hapa inaruhusiwa kufungua muda wowote.


2.Kutia nia ya safari baada ya alfajir. Yaani safari imetokea baada ya kuswali au mchana. Hapa maulamaa wengi wamesema mtu hataruhusiwa kufungua. Ila kwa uchambuzi zaidi uliofanywa juu ya safari za mtume na mapokezi mengi ni kuwa inafaha kufungua muda wowote na hii ndio kauli yenye nguvu.


3.Mtu kutia niya ya kufunga akiwa safarini na baadaye kutia niya ya kufungua. Hapa inajuzu kufungua.


Muda wa kufungua safarini.


Pindi msafiri atakapokusudia kufanya makazi ya kudumu basi hapa ruhusa ya kufungua inakatika. Ila kama hajakusudia kufanya makazi ya kudumu ataendelea kutofunga. Amesimulia Ibn 'Abas kuwa 'hakuacha Mtume kuendelea kutofunga (kula) mpaka ukakatika mwezi' (Bukhari).


Na pindi akirudi katika makazi yake usiku atafunga siku inayofata. Ama akirudi katikati ya mchana hapa maulamaa wapo walosema atajizuia kula na kunywa. Ila kauli yenye nguvu ni kuwa ataendelea kula kama alivyokuwa safarini. Ila stara ya kula izingatiwe. Ibn Mas'ud amesema kuwa: mwenye kula mwanzoni mwa mchana, basi na aendelee mapaka mwishoni' (Ibn Abi Shayb)


3.wazee (vikongwe).


Wazee sana yaani vikongwe ni ruhusa kwao kutofunga. Ila pia wakitaka wanaweza kufunga. Na kama wakitofunga hawatakiwi kujalipa funga ila watalisha masikini katika kila siku ambayo hawajafunga kulisha masikini..


4.mgonjwa ambaye ugonjwa wake hautarajiwi kupona hukumu yake ni sawa na ya wazee au vikongwe.


5.Mwenye mimba na mwenye unyonyesha.
,as-aa hii ni katika mas-al zeny utata sana kwa maulamaa. wapo waosema akifungua mweny mimba au menye kunyonyesha kwa kuhofia afya ya mototo aidha kutopata maziwa au kudhoofu kwa afya ya mtoto aliyepo tumboni basi hapa hukumu ni kufungua na kulisha masikni kwa kila siku ambayo hatafunga. Na itawalazimu baadaye kujalipa. A ikitoea hawakufunga kwa ajili ya kuhofia afya zao kua kama watafunga huenda wkaumwa basihapa hukumu ni kutofunga ila itawalazimu kujalipa badae bila ya ulisha masiini.


Baada ya uchamuzi wa kina juu ya hadthi mbalimbali maulamaa wengine wameona watu hawa wnaruhuswa kufungua na watalisha masikini kwa kila sikuambayo haakufunga na hakuna haja ya kuja kulipa. Na huu ndio msimamo wenye nguvu zaidi. Na masahaba wengi walikuwa wakiamini hivi akiwemo Ibn 'Abas na Ibn 'umar.


Maulamaa hawa wanatoa hoja hizi:-


1.amesema Ibn Abas kuwa (hadithi ni ndefu ila ndani yake akasema ) '.mwenye mimba au mwenye kunyonyesha watakapohofia watalisha kila siku makisini' (hadithi hii ni sahihi na ameipokea Bayhaqiy).


2.Amesimulia Nafi'i kuwa '.alikuwepo binti mmoja mwenye mimba na akapiga chafya katika mwezi wa ramadhani basi Ibn 'Umar akamuamrisha afungue na badala yake alishe katika kila siku masikini' (hadithi hii ni sahihi na ameipokea Drqutniy)


2.watu ambao ni wajibu kufungua na wanatakiwa walipe.
1.Hawa ni watu aina mbili nao ni wenye heddhi au nifasi. Hawa ni lazima kufungua na watalipa siku hizi baada ya ramadhani na kabla ya kuingia ramadhani nyingine. Na akitwaharika mwanamke ndani ya mchana wa ramadhani ataendelea na kula kwake. Na akitwaharika kabla ya alfajiri na akawa ametia niya ya kufunga itasihi funga yake na ijapo atachelewa kuoga. Mtu mwenye damu ya ugonjwa ataendelea kufunga.


2.Kwenye kuhofia maangamivu kwa kufunga. Yaani pindi akiwa mtu katika hali ambayo akifunga huenda akafariki au kupata matatizo makubwa sana basi mtu huyu ni wajubu kwake kufungua.


3.ambao haijuzi kufungua
Ni kila muislamu aliye balehe na kuwa na akili timamu, mkazi wa mji na asiwe mgonjwa.


Kulipa funga ya ramadhani
1.maulamaa wanazungumzia kuwa aliyefungua katika mwezi wa ramadhani atawajibika kuilipa fungaile. Na Allah ndiye anajua zaidi. Kuna kauli kuwa Ibn Mas'ud amesema kuwa: mwenye kufungua mwezi wa ramahani bila ya udhuru wala ruhusa haitatosha kulipa funga ile hata akifunga mwaka mzima' (hadithi hii ni sahihi na ameipokea Ibn Abi Shaiba)


2.Kulipa funga ya ramadhani sio lazima kuilipa kwa haraka. Unaweza kuchelewesha kadiri uwezavyo ila isikutane na ramadhani nyingine. Amesema Aisha kuwa: 'nilikuwa ninakaa na madni ya funga za ramadhani na nilikuwa siwezi kuzilipa mpaka unaingia mwezi wa shaaban' (Bukhari na Muslim)


3.Ikitokea mtu amekaa na deni la funga mpaka ikaingia ramadhani, hapa atatakiwa kufunga ramadhani na atakuja kulipa atakapomaliza kufunga ramadhani. Yaani kuanzia shawal.


4.Hakuna haja ya kufululiza katika kulipa ramadhani. Yaani ukiwa unalipa unaweza kufunga na kuacha na kuendelea mpaka umalize.


5.Mwenye kufa akiwa na funga hapa kuna tofauti ya kauli kwa maulama. Lakini jambo amablo lip[o wazi ni kuwa


A)ikiwa amekufa akiwa amekufa na udhuru wa kutofunga huyu hatalipiwa funga zake.


B)Akifa na hukuwa hana udhuru wa kutolipa deni lake na akafa bila ya kulipa deni hapa watamfungia warithi wake.


C)Akifa huku ana nadhiri ya kufunga, hapa watamfungia warithi wake.


USIKU WA LAYLAT AL-QADIR.
FADHILA ZA USIKU HUU
Allah ameiteremsha Quran kwenye usuku huu. Allah amesema 'hakika sisi tumeitetemsha (quran) katika usiku wa laylat al-qadir' (quran 92:1) Allah ametukuza sana ukisu huu hata akasema kuwa ni mbora kuliko miezi elfu moja. Allah amesema '(siku wa) laylat al-qadir ni mbora kuliko miezi elfu moja (quran 97:3)


Hushuka malaika ndani ya usiku huu, na jibrili akiwemo. Pia maulamaa wamsema kuwa maana ya aya hii ni kuwa hushuka malaika na rehema, baraka na utulifu. Pia wamesema maulamaa kuwa hushuka malaika na kila amri ambayo Allah ameihukumu katika mwaka mzima huu kama alivyosema Allah katika surat dukhan aya ya 4-5.


Amani hushuka ndani ya usiku huu kuwashukia waumini mpaka alfajiri.


Amesimulia hadith Abuuhurairah kuwa mtume (s.a.w) amesema 'mwenye kufunga ramadhani kwa imani na kutaraji malipo kwa Allah atasamehewa madhambi yake yalotangulia. Na mwenye kusimama katika usiku wa laylat al-qadir (akifanya ibada) kwa imani na kutaraji malipo kwa Allah atasamehewa madhambi yake yalotangulia. (Bukhari na Muslim).


NI UPI USIKU HUU?
Hakuna shaka juu ya kuwa usiku huu unapatikana kwenye mwezi wa ramadhani kama Alivyosema Allha kuwa ameiteremsha quran kwenye usiku huu,(quran 97:1). Na amesema pia kuwa mwezi wa ramadhani ndio mwezi ambao qurani imeteemshwa.(quran 2:185).


Na Ibn Hajar amezungumza kuwa maulamaa wametofautiana juu ya kuutambua usiku hii ni wa mwezi ngapi?, kauli zao zinafika mpaka 40. Miongoni mwa kauli hizo ni kama:-


1.maulamaa wengi wamekubaliana kuwa usiku huu unapatikana katika kumi la mwisho la mwezi wa ramadhani. Kauli hii inaegemea hadithi aloisimulia Abuu Sa'id al-khudriy kuwa Mtume (s.a.w) amesema '.utafuteni (usiku wa laylat al-qadir) katika kumi la mwisho' (Bukhari na Muslim)


2.na maulamaa wengi wamekubaliana kuwa usiku huu unapatikana katika masiku yaliyo witir kwenye kumi la mwisho yaani mwezi 21, 23, 25, 27, na 29. Maelezo haya yanaegemea kauli ya Mtume aliposema 'kesheni kuutafuta usiku wa laylat al-qadir katika masiku yaliyo witiri katika kumi la mwisho' (Bukhari)


3.na kauli za maulamaa wengi wamekubaliana kuwa usiku huu ni wa mwezi 27. Na kauli hii ndiyo pia walivyokuwa wakiamini wengi katika maswahaba (Allah awaridhie wote) na kauli hii pia inaegemea hadithi sahihi kama alivyopokea Muslim na Tirmidh)


Jambo la ufupi ni kuwa usiku huu kwa hakika haujulikani kuwa ni upi ila bila shaka upo kumi la mwisho katika masiku yaliyo witir. Mtume amesema kuwa: 'mimi niliuona usiku wa laylat al-qadir kisha nikasahau.'.' (Bukhari na Muslim)


Usiku huu umefichwa ilikwamba tujibidiishe kumuabudu Allah sana katika kumi lote la mwisho. Mtume (s.a.w) alikuwa akikesha usiku kufanya ibada kumi la mwisho .na alikuwa aliwaamsha wakeze kufanya ibada katika kumi hili la mwisho. Usiku huu umefichwa na mtume alipoujua alitaka kuwaeleza maswahaba na akasahau. (Bukahari)


NINI MTU AFANYE KATIKA USIKU HUU?
1.kusimama kwa ajili ya ibada
Mtume alikuwa lifikapo kumi la mwisho akijitahidi sana kufanya ibada kuliko nyakati zingine. (Buhari na Muslim). Mtume alikuwa akikaza msuli wake na kujifunga nguo kisawasawa, na alikuwa akikesha na akiwaamsha wakeze (watu wa familia yake kufanya ibada usiku) (Bukhari na Muslim)


2.kuomba dua na adhkar mbalimbali
Imesimuliwa kuwa 'Aisha (r.a) alimuuliza Mtume amfundishe nini aseme katika usiku wa laylat al-qadir Mtume akamjibu sema 'ALLAHUMMA INNAKA 'AFFUWUN TUHIBUL-'AFWA FA'AF-'ANNI' (Tirmidh na Ibn Majah)


ALAMA ZA USIKU HUU
1.hakuna upepo unaovuma na anga lake hutulia na jua huchomoza likiwa dhaifu (halichomi)
2.Kunakuwa na utulivu
3.Wajawema wanaweza kuuona kwenye ndoto
4.Jua litachomoza asubhi likiwa safi na halichomi


ZAKAT AL-FITR
Hii ni zaka inayotolewa kwa ajili ya fitr. Yaani huliwa sikuile ya kufungua kutoka kwenye funga ya ramadhani. Hutolewa kwa kuwatosheleza wale wenye shida ya shakula na kuingiza furaha kwa wasiojiweza siku ya 'idi na pia ni kwa ajili ya kutakasa funga za walofunga mwezi wa ramadhani. Funga hutakaswa kwa yale yalotuponyoka na tukafanya maovu katika mwezi wa ramadhani. (Abuu Daud na Ibn Majah ). Pia zaka hii hutolewa kabla ya kutoka kwenye swala ya 'id na mwenye kuitoa baada ya swala ya 'id itakuwa ni sadaka kama sadaka zingine na si zaka. (Abuu Daud na Ibn Majah kwa isnad sahih).


Hukumu ya zaka hii ni faradhi kama ilivyokuja kauli kuwa Ibn 'Umar amesema: 'amefaradhisha Mtume (s.a.w) zaka ya fitir pishi la tende au ngano kwa mtumwa na kwa huru wanaume na wanawake, watoto na wakubwa katika waislamu na akaamrisha itekelezwe kabla ya kutoka kwenye swala ya 'id (Bukhari na Muslim).


JUU YA NANI INAMUAJIBIKIA ZAKA YA FITIR
1.kila muislamu kama hadithi ya hapo juu ilivyo taja
2.Mwenye kuweza juu ya kutoa zaka hii


Zaka hii hutolewa kiasi cha kilo mbili na nusu (2.5) kwa kipimo cha juu. Wapo walosema mbili na robo. Pia hutolewa chakula ambacho hupendwa kuliwa eneo lile kwa kauli za maulamaa. Kwa mfano kwetu Tanzania ni Mchele. Pia utawapa watu wasiojiweza kama masikini. Maulamaa pia wamejuzisha kutoa pesa kwa hesabu ile ya zaka hii.



Pata kitabu Chetu Bofya hapa



Je! umeipenda hii post?
Ndio            Hapana            Save post

Kama unahitaji kuuliza maswali Bofya hapa

Mwandhishi Tarehe 2018-08-01     Share On Facebook or Whatsapp Imesomwa mara 524


Download our Apps
👉1 Kitau cha Fiqh     👉2 Madrasa kiganjani     👉3 kitabu cha Simulizi     👉4 Kitabu cha Afya    

Post zifazofanana:-

tarekh 06
MAISHA YA UTOTONI YA MTUME S. Soma Zaidi...

DARSA ZA NDOA, FAMILIA, SIASA, BIASHARA, UCHUMI, HAKI NA SHERIA KATIKA UISLAMU
1. Soma Zaidi...

Umuhimu wa swala
Umuhimu wa KusimamishaSwala Kwa mujibu wa Hadith ya Ibn Umar (r. Soma Zaidi...

Masharti ya swala
Sharti za SwalaSharti za Swala Sharti za swala ni yale mambo ya lazima anayotakiwa Muislamu ayachunge na kuyatekeleza kabla hajaanza kuswali. Soma Zaidi...

Kuamini mitume wa mwenyezi Mungu, sifazao na lengo la kuletwa kwao
1. Soma Zaidi...

Sababu za kushuka kwa Surat al-Kawthar na fadhila zake
SURATUL-KAUTHAR Imeteremshwa maka, na sura hii imeshuka kwa sababu al-aAs ibn Waail. Soma Zaidi...

'Allah (s.w) humwingiza katika rahma zake amtakaye na kumwacha kupotea amtakaye'
Soma Zaidi...

Je mahari inashusha hadhi ya mwanamke?
Je, Mahari inashusha hadhi ya mwanamke? Soma Zaidi...

Kuepuka Maongezi yasiyo na Maana
12. Soma Zaidi...

vita vya ahzab, sababu ya kutokea vita hivi na mafunzo tunayoyapata
Vita vya Ahzab- Maquraish waliungana na mayahudi, wanafiki na makabila mengine ya waarabu baada ya kuona kuwa wao peke yao hawawezi kuufuta Uislamu. Soma Zaidi...

Utaratibu wa kutekeleza hija, matendo hatua kwa hatua, pamoja na kusherehekea sikuku baada ya hija
4. Soma Zaidi...

DUA 51 - 60
51. Soma Zaidi...