QURAN: TAJWID, FADHIKA ZA KUSOMA QURAN, FADHILA ZA KUSIKILIZA QURAN, FAIDA ZA SURAT FATIHA, YASIN, BAQARA, TABARAK

QURAN: TAJWID, FADHIKA ZA KUSOMA QURAN, FADHILA ZA KUSIKILIZA QURAN, FAIDA ZA SURAT FATIHA, YASIN, BAQARA, TABARAK

Darsa za Quran

Ustadh Rajabu

DARSA ZA QURAN

DARSA ZA QURAN
Sifa njema zinmstahikia Allah Mola wa ulimwengu, sala na amani zimuendee Mjumbe wa Allah Mtume wetu Muhammad (s.a.w). Ama baada ya utangulizi huu; huu ndi mwendelezo wa darsa za quran ambapo tutajifunza mambo mengi kuhusu quran na dini yetu. Kabla ya kuendelea mbele zaidi inabidi kwanza tufahamu baadhi ya maneno kadhaa. Tujie kwamba quran imetujia sisi kutoka hapo ilipoandikwa kuja kwa Mtume kupitia malaika jibril.


Tumeamuwa kuandika makala hii fupi
Maana ya Wahyi.


Ni ufunuo kutoka kwa Allah (s.w) kwenda kwa wanaadamu (mitume) kupitia Malaika wake Jibril (a.s). Wahyi umegawanyika katika makundi makuu mawili ambayo ni Qurani na Hadithi. Wahyi umekuwa ukimjia Mtume na mitume wengine walotangulia kupitia malaika jibril. Lakini zipo njia nyingine ambazo wahyi unaweza kuwajia wanadamu. Njia hizo ni;-
1.Il-hamu
2.Kusemeshwa na Allah (s.w) nyuma ya pazia.
3.Kupitia malaika.
4.Ndoto za kweli.
4.Maandishi.


- Qur'an ni maneno ya Allah (s.w) yaliyoteremshwa kwa Mtume (s.a.w) kwa njia ya wahyi kupitia Malaika Jibril (a.s) ili kuwa mwongozo kamili wa maisha ya wanaadamu. Qurani imekuwa ikitambulika kwa majina mengi sana yakiwemo;-


Al-Qur'an ' Chenye kuunganishwa pamoja au chenye kusomwa.
Kalamullah ' Maneno ya Mwenyezi Mungu (s.w).
Al-Mas-haf ' Mkusanyiko wa kurasa nyingi (Kitabu kikubwa).
Al-Kitabu ' Kitabu Pekee (The Unique Book) Kimuundo, Kimaudhui,


Kiusahihi, n.k.


Al-Furqaan ' Kipambanuzi baina ya haki na batili.


Adh-Dhikru ' Mawaidha au Ukumbusho.


At-Tanziil ' Kiteremsho (Mshuko), Wahyi kutoka kwa aliye juu.


Al-Hukmu ' Kitabu pekee kinachostahiki kumhukumu binaadamu.


Al-Hikma ' Kitabu pekee chenye hikima isiyo na kikomo (Kitabu cha Hikima).


Ash-Shifau ' Ponyo au dawa pekee ya kuponya nafsi, nyoyo, uasi, ukafiri, n.k.


Ar-Rahma ' Rehema kwa wanaadamu.


Al-Khayr ' Kheri pekee, Qur'an ndio chanzo cha kheri zote.


Ar-Ruuhu ' Roho ya maisha, asiyeishi kwa mujibu wa Qur'an ni maiti.


Al-Bayaana ' Chenye kuweka wazi, kubainisha kila kitu kwa uwazi, n.k.


An-Nuur ' Nuru peke ya kumuangazia binaadamu katika njia sahihi ya maisha.


Al-Burhan ' Hoja zilizo wazi, zenye kueleweka kwa kila mwenye akili.


Al-Haqq ' Kitabu cha Haki, kinachotoka kwa Mola wa Haki kwa ajili ya Kusimamia haki.


Ahsanul-Hadith ' Simulizi, maelezo, hadith nzuri kuliko zote.


Al-Hudaa ' Mwongozo pekee sahihi wa maisha ya mwanaadamu.


Qur'an ni Kitabu chenye aya 6,236, zilizo katika sura 114 na kimegawanywa katika Juzuu (mafungu) 30. Pia inatupasa tujuwe kuwa qurani kabla ya kumfikia mtume ilipitia hatuwa kuu mbili a,bazo ni;-


Qur'an imeshuka katika hatua kuu mbili;


1.Imeshuka jumla kutoka Lawhim-Mahfuudh (Ubao uliohifadhiwa katika Arshi) hadi Mbingu ya Dunia.


2.Kushuka kidogo kidogo duniani kuja kwa Mtume (s.a.w) kupitia Malaika Jibril (a.s) kwa muda wa miaka 23. Rejea Qur'an (85:21-22), (81:19-20)


Mtume (s.a.w) alianza kushukiwa na wahyi wa kwanza wa Qur'an mwaka 610 A.D akiwa na umri wa miaka 40 katika pango la 'Jabal Hiraa'. Qur'an ilianza kushushwa katika mwezi mtukufu wa Ramadhani katika Usiku wenye cheo wa 'Lailatul ' Qadri'. Rejea Qur'an (97:1-5) na (2:185). Ilianza kushuka kwa aya 5 za mwanzo katika suratu Alaq (96:1-5).


MGAWANYIKA KATIKA QURAN.


Wataalamu wa elimu za Qurani katika fani za uandishi na usomaji wameigawanya Qurani katika mafungu ili kuwezesha urahisi kwa wasomaji wa qurani. Katika Darsa hii tutaangalia migawanyiko hii.


Sura katika qurani zimegawanywa katika makundi makuu mawili:


1.sura zilizoteremshwa Makka na na huitwa Maki


2.Sura zilizoteremshwa Madina na huitwa madani


Sura hizi unaweza kuzijuwa kwa mujibu wa kanuni na taratibu ambazo zimewekwa na maulamaa wa elimu za Quran. Ila kwa ufupi ni kuwa Sura za makka ni zile ambazo zimeteremshwa kabla ya mtume (s.a.w) hajamaliza hijra kufika madina na zile za madina ni zile ambazo zimeshushwa wakati mtume (s.a.w) amesha hama kwenda madina.


Utofauti wa sura hizi ni kuwa nyingi katika sura zilizoshushwa Maka ni fupi na Maudhui yake yamejikita sana katika kuboresha imani. Na zile za Madina zina sifa ya kuwa ndefu na maudhui zake nyingi zimekuwa zikizungumzia hukumu na sheria.


Pia qurani nzima imegawanywa katika vipande vipande kama ifuatavyo 1.Juzuu 30 3.Rukuu(paragraph)
4.Aya
5.Manzil


Aya ni umoja na wingi wake ni Ayat. Ni vigumu kufasiri neno Aya kwa kiswahili ila kwa ufupi unaweza kusema ni sentesi ijapokuwa maana hii ni tofauti kidogo ila angalau inaleta maana. Aya katika Qurani zipo 6236. Na aya ndani ya Qurani inaweza kutengenezwa na mkusanyiko wa maneno au herufi. Pia aya inaweza kuwa herufu mojatu na ndo maana ni tofauti na neno sentensi kwa kiswahili.


Sura katika qurani zipo 114 na sura zote zimeanzwa na basmala isipokuwa sura ya 9 surat trauba yenyewe haina basmala. Kuna sababu nyingi zinatolewa na na wajuzi katika elimu za Quran kuelezea kwa nini sura hii haijaanzwa na basmala. Ila kwa ufupi ni kuwa hakukupatikaniwa dalili ya kufanya hivyo kutoka kwa mtume(s.a.w). Tutazungumzia zaidi mas-ala hii katika asbab-nuzul. Halikadhalika basmala kwenye qurani zipo 114 kuna sura moja ina basmala 2 nayo ni surat an-namli ambayo ni sura ya 27. Sura kwenye qurani zimepangiliwa kuanzia 1 mpaka 114. Ila mpangilio huu sio kulingana na kushuka kwao.


Rukuu ni mgawanyiko mwengine. Kwa kiswahili rukuu ni aya. Rukuu wingi wake ni rukuu'at na huweza kutengenezwa na muunganiko wa aya nyingi ambazo zote zinazungumzia maudhui moja. Katika qurani kuna rukuu 558. Alama ya rukuu ni herufi ' kubwa. Alama hii ina sehemu kuu 3 juu kati na chini.


1.juu huwekwa namba ya rukuu kuwa ni ya ngapi kwenye sura 2.Kati huwekwa namba za aya zilizomo kwenye hiyo rukuu
3.Huwekwa namba ya rukuu kuwa ni ya ngapi kwenye Quran


Juzu zipo 30 katika qurani yote. Hii ni rahisi kwa watu wanaotaka kumaliza kusoa qurani katika mwezi mmoja yaani ndani ya sikun 30. Kwa mashafu za kuhifadhisha qurani kila juzu inakuwa na kurasa 10 isipokuwa zujuu 'Amma ambayo ndo juzuu ya 30 yenyewe ina kurasa zaidi.


Manzil wingi wake ni manaazil. Qurani imegawanywa katika manazil saba 7. Hii huwezesha urahisi kwa wanaotaka kumaliza kusoma qurani ndani ya wiki moja yaani siku saba 7. Manaazili huandikwa namba zake nyingi ya ukingo wa kurasa ya mashaf.


1.Manzil 01 huanzia sura ya 1 hadi ya 4 2.Manzil 02 huanzia sura ya 5 hadi ya 9
3.Manzil 03 huanzia sura ya 10 hadi ya 16
4.Manzil 04 huanzia sura ya 17 hadi 25
5.Manzil 05 huanzia sura ya 26 hadi 36
6.Manzil 06 huanzia sura ya 37 hadi 49
7.Manzil 07 huanzia sura ya 50 hadi 114


FADHILA (UMUHIMU) WA KUSOMA QURAN.
1.quran ni kamba,ponyo,kinga,nuru na ni kitu chenye kuokoa.
Kwa ufupi unaweza kusema qurani ina kila kitu ambacho tunakihitajia katika maisha yetu. Qurani inaweza kutumika kama tiba ya kuondoa maradhi ana kinga dhidi ya maradhi, uadui na husda. Pia ni nuru inayoweza kumuongoza mtu wapi apite.


Qurani humkinga mtu na maadui, maradhi, husda na kila kitu kubada. Maneno haya unaweza kuyakuta katika hadithi ndeefu aliyoipokea al-haakim katika mapokeza ya 'Ablahhah Ibn Mas'ud kuwa Mtume amesema 'hakika hii qurani ni kamba ya Allah, na ni nuru iliyo wazi, na ni pozo lenye kunufaisha, na ni ngome (ya kujikinga) kwa mwenye kushikamana nayo na ni kitu chenye kuokoa kwa mwenye kuifuata.'..'


2.Qurani ni yenye kuombea shifaa siku ya qiyama. Watu watakuwa katika hali na wakati mgumu siku ya qiyama. Katika tabu za namna hiyo qurani itakuwa ni yenye kuwaombea watu wake wapate shifaa mbele ya Allah. Amasimulia Abuu Umamah kuwa 'nimemsikia Mtume akisema 'isomeni qurani, kwani hakika itakuja siku ya kiyama hali yakuwa ni yenye kuwaombea watu wake' (amepokea Muslin)


3.Ukisoma herufi moja unaandikiwa mema (thawabu) 10. Amesimulia Ibn msud kuwa mtume amesema 'mwenye kusoma herufi moja katika kitabu cha Allah atapata jema moja, na jema moja hulipwa kwa mara kumi kwa mfano wake.'(amepokea Tirmidh). Katika muendelezo wa hadithi Mtume anasema ukisema ALM hizi ni herufi tatu, hivyo kila moja hulipwa kwa kumi.


4.Wenye kusoma qurani ndio watu bora. Mtume amewapa nafasi kubwa sana watu ambao wanaisoma qurani. Katika masimulizi ya 'Uthman Ibn ;Afan mtume amesema 'mbora wenu ni yule mwenye kujifundisha qurani kisha akaifundisha.' (amepokea Bukhari, Abuu Dauw na Tirmidh).


5.Mtu atapandishwa darsa kwa kiasi alichohifadhi qurani peponi. Watu watakapoingia peponi watapandishwa madaraja ya peponi kulingana na kiasi cha mtu anachoweza kusoma katika qurani. Amesimulia Abdallah Ibn Umar kuwa Mtume amesema ataambiwa mtu aliyeisoma qurani (akiwa peponi) soma na upande darja na uisome kama ulivyokuwa ukiisoma ulivyokuwa dunianai. Kwa hakika makazi yako yataishia pale itakapoishia aya ya mwisho utakayoisoma'. (amepokea Abuu Dawd na tirmidh).


6.Mwenye kusoma vizuri qurani atakuwa na malaika. Amesimulia Aisha kuwa mtume amasema mwenye kusoma qurani na akawa mahiri nayo (anaisoma vizuri) atakuwa pamoja na malaika wema wenye kutii. Na yule mwenye kuisoma na akawa anakwamakwama (hajaiweza vizuri na anajitahidi aiweze) na huku anashaka atapata malipo mara mbili' (amepokea bukhari, Muslim na wengine).


TAHADHARI KWA WASOMAJI WA QURANI
Mtume ameamrisha watu waihifadhi qurani. na sihivyo tuu Mtu aliyehifadhi qurani ajitahidi anafanya jitihada isije akaisahau. Katika hadithi sahihi Mtume anazungumzia kuwa qurani itakimbia kama inavyokimbia kamba ya ngamia.


Kusahau qurani baada ya kuihifadhi ni katika madhambi. Hivyo wasomaji wa qurani tujitahidini kuihifadhi na kuhakikisha pale tulipopahifadhi tunapashikilia pasiondoke. Amesimulia Anas ibn Maliki kuwa Mtume amesema 'nilioneshwa malipo ya uma wangu (nikaona kuna malipo ) mpaka kwenye uchafu anaouondoa mtu msikitini. Na nilioneshwa madhambi ya uma wangu, basi sikuona dhambi kubwa kuliko sura katika qurani au aya aliyopewa mtu kisha akaisahau' (amepokea Abuu Dauw, Tirmidh na Ibn Majah).


ADABU ZA KUSOMA QURANI
1.kuwa na ikhlas. Hapa jinachokusudiwa ni kuwa na nia iliyo takata kuwa unasoma kwa ajili ya Allah na si vinginevyo. Kama ilivyokuwa ibada zote anatakiwa afanyiwe Allah kama Mtume alivyosea katika hadithi sahihi aliyoipokea Bukhari, Muslim kwa mtume amesema 'hakika si vinginevyo amali (hulipwa) kwa (kuzingatia) nia...' . Hivyo msomaji asifanye ili watu wamsikie eti yeye ndo bigwa ila asome kwa kutaraji radhi za Allah.


2.Kuwa na khushui, na kuleta mazingatio. Mwenye kusoma qurani ajitahidi ahudhurishe moyo wake wote kwenye lile analolifanya nalo ni kusoma qurani. Pia alete mazingatio kama anaelewa nini qurani inazungumza. Amesema Ibraahim Khawas kuwa: dawa ya nyoyo ni mambo matano ambayo nui: kusoma Qurani kwa mazingatio, kufunga, kusimama usiku na kukaa na watu wema.


3.Kulia wakati wa kusma Qurani. Mwenye kusoma qurani huenda ikamfanya alie, hivi ni vizuri sana na ni sifa ya watu wema. Hata mtume alikuwa naposomewa qurani alikuwa akilia.


4.Kusoma kwa sauti. Mzomaji wa qurani anatakiwa atoe sauti yake yaani asome kwa sauti kwa namna ambayo hatawaudhi watu walio karibu nae kama mtu aliolala, anayeswali ama waliokuwepo kwenye mazungumzo yake.


5.Kusoma kwa sauti nzuri. Msomaji wa qurani anatakiwa ajitahidi kuwa na sauti nzuri. Zipo riwaya nyingi ambazo zinaonesha msisitizo juu ya kuremba sauti. Mapaka mtume akasema 'mtu amabye hasomi qurani vizuri sio katika sisi.' katika mapokezi mengina ya Bukhari, muslim na Abuu Dawd ni kuwa Allah amemuamrisha mtume kusoma qurani kwa sauti nzuri.


6.Tajweed. Maana ya tajweed ni kuisoma qurani kwa hukumu zake. Qurani ina hukumu zake katika kusoma. Kila herufi inatakiwa itamkwe kwa namna ileile inayotakiwa. Kila herufi ipewe haki yake katika idh-hari, ikh-fai, id-ghami, mada, ghunnah na ntingineso nyingi.


7.Kudhihirisha maana. Mwenye kusoma qurani ajitahidi kudhihirisha maana wakati anaposoma. Mtu anatakiwa ajuwe kitu ambacho kinazungumziwa katika aya anayoisoma.


8.Kusoma kwa kupumzika. Kwenye kusoma qurani natakiwa asisome mfululizo ila awe ana viu vya kupumzika. Amesimulia Ummu salama kuwa alikuwa mtume anapumzika kwenye usomaji wake alikuwa akisoma AL-HAMDU LILLAHI RABIL-ALAMIIN kisha hupumzika kisha anasoma AR-RAHMAANIR-RAHIIM kisha hupumzika, kisha husoma MALIKI YAUMIDIIN (amepokea Tirmidh).


9.Kuchunga hukumu za waqfu. Waqfu unaweza kusema ni vituo vya kupumzikia au kutokupumzika au kuunga maneno wakati wa kusoma qurani. Kuna ambavyo inajuzu kuunganisha ('), au kujuzu kusimama ('), au kujuzu kusimama ila kwa ufupi ('), au vya lazima kusimama (') au ambavyo haitakiwi kusimama (').


10.Kutokusoma harakaharaka (mbiombio). Basi mwenye kusoma Qurani ajitahidi kusoma katika mpangilio unaopendeza. Sio mbiombio kiasi kwamba inaweza kuwa rahisi kufanya makosa ya kiusomaji.


11.Inapendeza pia kutwaharisha kinywa kwa kupiga mswaki kabla ya kusoma qurani.


12.Kusoma kwenye msahafu. Hili ni jambo ambalo linapendeza kwa wale wanaotaka kuhifadhi qurani. Tofauti na kusikiliza ikisomwa wawe wanaangalia maandishi ya qurani hasa kwenye msahafu.


13.Kumuomba Allah unaposoma qurani. Amesema Mtume 'mwenye kusoma qurani basi na amuombe Allah kwayo, kwani hakika watakuja watu watasoma qurani na wataomba kwayo watu' (amepokea tirmidh)


14.Msomji awe ni twahara. Hili ni jambo linalipendeza sana kwa anayesoma qurani awe na tahara. halikadhalika mtu mwenye janaba haruhusiwi kusoma qurani ila kama ataisoma kama dua. Kwa mfano akisoka adhkari za kulala ambazo zina qurani ndani yake.


15.Kuanza kusoma qurani kwa kujikinga na shetani yaani kusema 'A'UDHU BILLAHI MINAS-SHAYTWANIR-RAJIIM'


16.Kuomba dua unapofika sehemu za heri. Amepokea hadithi Muslimu kuwa Abuu 'Abdallah Hudhaifiya amesimulia kuwa alikuwa Mtume ' Anaposoma aya yenye tasbih huleta tasbih, na anaposoma aya yenye maombi(dua) huomba (dua), anaposoma aya yenye t'awdh (kutakahifadha) hutaka hifadha'


17.Kujikinga na shari anaposoma aya za shari. Yaani anaposoma aya ambazo zinataja adhabu za makafiri na watu waovu humuomba Allah amuepushe kuwa katika kundi hilo.


18.Kleta sijdat tilawa unapofika sehemu za kusujudi.


ADABU ZA KUSIKILIZA QURANI
1.kutafuta msomaji mwenye sauti mzuri. Inapendeza mtu mwenye kusikiliza qurani asikilize kwa yule mwenye sauti ambayo ataipenda. Jambo hili litampa hamu ya kusikiliza qurani. Hata mtume alikuwa na wasomaji wake maalumu wa kumsomea qurani. Amesimulia Jabir kuwa mtume amesema 'hakika mtu mwenye sauti nzuri anaposima qurani ni yule ambaye pindi mnapomsikia anasoma qurani mnamdhania kuwa anamuogopa Allah. (amepokea ibn majah).


2.Kuleta mazingatio pamoja na kufikiri kwa kina maana. Inatakiwa nayesikiliza qurani sio tu atosheke na sauti lakini anatakiwa awe na mazingatio juu ya kile ambacho kinasomwa.


3.Mwenye kusikiliza qurani awe ni mzuri wa kusikiliza na mwenye kunyamaza. Amesema Allah kuwa 'na pindi inaposomwa qurani isikilizeni na nyamazeni ili mrehemewe. (surat al-a'araaf 204)


4.Kulia na kuwaidhika na kinachozungumzwa. Kama ilivyo kwa msomaji hata msikilizaji pia ni vema akalia kwa kuwaidhika na qurani. Amesema Allah 'na pindi wanaposikia yale yaliyoteremswa kwa Mtume utayaona macho yao yanabubujika machozikutokana na yale walioyajua katika haki' (surat maaidah 83)


5.Kuleta khushui, unyenyekevu na kutukuza kitabu cha Allah. Mwenye kusikiliza qurani ahakikishe kuwa analeta khushui na unyenyekevu, awe na utulivu huku akijuwa ukubwa wa kitabu cha Allah.


6.Kusujudi pindi unaposikia aya ya kusujudi. Sijida hii ni sunnah na mbele za maimamu wa fikh wapo wanaiita ni swala kama ilivyo swala ya jeneza. Hivyo haipasi mtu kusujudi akiwa hana udhu. Atasema mwenye kusujudi sijida hii 'SAJADA WAJHI LILLADHII KHALAQANIY WASHAQA SAM'AHU, WABASWARAHU, BIHAWLIHI, WAQUWATIHI' amsesimulia 'Aisha. Aya hizi za sijida zipo 15 katika qurani ambazo ni aya ya mwisho ya surat al-araf, aya ya 15 ya surat rad, aya ya 50 ya surat nahli, aya ya 109 ya surat israa, aya ya 58 ya surat maryam, aya ya 18 ya surat haj, aya ya 77 ya ryrat haj, aya ya 60 ya surat furqan, aya ya 26 ya surat naml, aya ya 15 ya surat sajda, aya ya 38 ya surat fusilat, aya ya 62 ya surat najmi, aya ya 21 ya surat inshiqaq, aya ya 19 ya surat 'alaq.


FADHILA ZA BAADHI YA SURA KWENYE QURANI
1.Surat al-fatiha.
Amesimulia Ibn 'Abas kuwa 'wakati ambao jibril alikuwa amekaa na Mtume akasikia sauti ya mlango uliofunguliwa juu yake akanyanyu kichwa chake kisha akasema 'hiyo ni nsauti ya mlango uliopo mbinguni umefunguliwa siku ya leo, na katu haujawahi kufunguliwa ila ni leo tu (ndio mara ya kwanza kufunguliwa). Basi akashuka Malaika kutoka kwenye mlango huu akasema (Jibril) 'huyu ni malaika ameshuka duniani na hajawahi kushuka kamwe ila ni leo tu' akatoa salamu (malaika huyo) kisha akasema (kumwambia mtume) 'toa habari za furaha kwa nuru mbili ulizopewa na hakuwahi kupewa mtume yeyote kabla yako kamwe (ambazo ni) surat al-fatiha na aya za mwisho za surat al-baqarah hatusoma herufi yeyote isipokuwa utapewa' (amepokea Muslim). Amesema Mtume 'surat al-fatiha ni dawa ya kila gonjwa' amepokea Bayhaqiy)


2.surat al-baqarah
Amesema Mtume 'Mwenye kuisoma katika nyumba yake usiku hatoingia shetani nyumba hiyo kwa muda wa siku tatu, na mwenye kuisoma mchana hatoingia shetani nyumba hiyo kwa michana mitatu' (amepokea Ibn hiban, tabrany na Bayhaqiy).


3.ayat al-qursiy.
Amesema Mtume 'katika surat al-baqarah kuna aya iliyobora kuliko aya zote haitasomwa aya hiyo kwenye nyumba yenye shetani ila atatoka kwenye nyumba hiyo, (aya hiyo ni) ayat al-kursy) (amepokea Al-Haakim na Bayhaqiy)


3.aya za mwisho za surat al-baqarah
Amesema Mtume hakika Allah ameimalizia surat al-baqarah kwa aya zilizo tukufu (zilizotoka) kwenye hazina chini ya 'arshi basi jifundisheni aya hizo na muwafundishe wake zenu na watoto wenu. Kwani mna ndani ya aya hizo dua, qiraa na dua' (amepokea Al-Haakim kutoka kwa Abuu Dhari).


Pia Amesema mtume 'aya mbili za mwisho za surat al-baqarah mwenye kuzisoma usiku zitamtosheleza' (amepokea bukhari,Muslim, Ahmad na Ibn Maajah kutoka kwa ibnmas'ud)


4.surat al-imraan
Amesema Mtume katika mafhumu ya hadithi iliyo sahihi kuwa itakuja qurani siku ya kiyama ikiongozwa na surat al-baqarah na al-imraan katika hali ya makundi mawili na yakawa yanajadiliana juu ya mtu wao yaani msomaji.


Pia amesema Mtume Mtu mwenye kusoma 'SHAHIDALLAHU ANNAHU LAA ILAAHA ILLAA HUWA WALMALAAIKATU WA-ULUL-ILMI QAAIMAN BIL-QISTWI LAA ILAAHA ILLAA HUWAL-AZIZL-HAKIIM. INNA DINA 'IN-DALLAHIL-ISLAM' Kisha akasema 'wa ana ash-hadu bimaa shahidaLLAHU bihi, wa astawdiu LLAHU hadhihi shahadah, wahiya lii indahu wadi'ah' Basi ataletwa mtu huyu siku ya kiyama na ataambiwa na Allah ewe mja wangu hii ni ahadi yangu niloahidi na mimi nina haki ya kutekeleza ahadi muingizeni mja wangu peponi' (amepokea Abuu Shaykh kutoka kwa Ibn masud).


5.surat israa
Amesema Mtume mwenye kusoma wakati wa asubuhi au jioni 'QULID-'ULLAHA AWID-'UR-RAHMANA AYAAMA-TAD-'U FALAHUL-ASMAAU-LHUSNAA' mpaka mwisho wa sura moyo wake hautokufa siku hiyo wala usiku huo. (amepokea Dilamy).


6.Surat Zumar Amesimulia 'Aisha kuwa alikuwa Mtume halali mpaka asome surat zumar na surat israa' (amepokea Tirmidh)7.surat alkahafi
Amesema Mtume 'mwenye kusoma surat al-kahafi siku ya ijumaa itampatia mwangaza kati ya ijumaa ile mpaka nyingine.(amepokea Al-haakim na Bihaqi kutoka kwa Abuu musa al-'Ashar). Amesema Mtume mwenye kuhifadhi aya 10 za mwanzo za surat al-kahafi atalindwa na fitna za Dajali.(mepokea Muslim, Ahmad,na Nisai kutoka kwa Abuu Drdaa).


8.surat yaasin.
Amesimulia Anas kuwa mtume amesema 'kila kitu kina moyo, na moyo wa qurani ni surat yaasin. Na mwenye kuisoma huandikiwa kwa kisomo chake thawabu za kusoma qurani mara kumi. (amepokea tirmidh na Dilamy).


Pia amesimulia Ma'aqil ibn yasar kuwa Mtume amesema 'moyo wa qurani ni surat yaasin, mwenye kuisoma kwa kutaraji radhi za Allah na mafanikio ya siku ya mwisho atasamehewa madhambi yake.' (amepokea imam Ahmad na Bayhaqi).


9.surat dukhani
Amesimulia Abuhurairah kuwa Mtume amesema 'mwenye kusoma surat dukhani wakati wa usiku ataamka asubuhi na huku malaika sabini elfu wakimtakia msamaha' (amepokea Tirmidh na nisai) na katika mapokeza ya Tabrani Mtume amesema 'mwenye kusoma surat dukhani siku ya ijumaa usiku au mchana Allah atamjengea mtu huyo nyumba peponi'


10.surat al-fat-hi
Amesimulia 'Umar kuwa Mtume amesema 'hakika imeshushwa kwangu mimi usiku wa leo sura ambayo ninaipenda kuliko vitu vyote vinavyochomozewa na jua' kisha akasoma INNAA FATAHNAA LAKA FAT-HAN MUBINAA (surat al-fat-hi) (amepokea bukhari).


11.surat al-waaqi'a
Amesimulia 'Abdullah ibn Mas'ud kuwa Mtume amesema 'mwenye kusoma surat al-waaqi'a kila usiku hatopatwa na njaa (kali) katu.


12.surat MUSBIHAT
Hizi ni sura zilizoanzwa na tasbihi yaani sabaha au yusabihu nazo ni tano ambazo ni al-hadid, al-hashri, swafa, al-jum-'a, na taghaabun. Amesimulia 'Irbaadh ibn Saariya kuwa hakika Mtume alikuwa akisoma musabihat kabla ya kulala na huwa akisema 'hakika mna katika sura hizo aya bora kuliko aya elfu moja' (amepokea tirmidh)


13.surat al-mulku
Amesimulia Abuuhurairah kuwa mtume amesema 'katika qurani kuna sura ina aya 30. Ni yenye kumuombea mtu mpaka atasamehewa nayo ni 'TABAARAKAL-LADHII BIYADIHIL-MULKU'. (amepokea Abuu Dawd na tirmidh)


14.Suratul ikhlas, nasi na falaq Amesimulia 'Abdallah Ibnhabib kuwa Mtume amesema 'QUL HUWA LLAHU AHADU na mu'awadhatayn (qul
a'udhu birabin-nasi na qul a'udhu birabil-falaq) (mwenye kuzisoma ) asubuhi na jioni zinatosheleza kwa kila kitu.(amepokea ahmad, Tirmidh na Nisai).



Pata kitabu Chetu Bofya hapa



Je! umeipenda hii post?
Ndio            Hapana            Save post

Kama unahitaji kuuliza maswali Bofya hapa

Mwandhishi Tarehe 2018-08-01     Share On Facebook or Whatsapp Imesomwa mara 500


Download our Apps
👉1 Madrasa kiganjani     👉2 Kitau cha Fiqh     👉3 kitabu cha Simulizi     👉4 Kitabu cha Afya    

Post zifazofanana:-