Chanzo cha vita vya Siffin na matokeo yake: Vita vya Ally na Muawia

Chanzo cha vita vya Siffin na matokeo yake: Vita vya Ally na Muawia

Vita Kati ya Khalifa Ali na Gavana Muawiya



Vita vya pili vya wenyewe kwa wenyewe ni vile vilivyopiganwa baina ya Khalifa Ali na Gavana Amir Muawiya wa Syria - vita hivi vinaitwa Vita vya Siffin.


Sababu hasa ya vita hivi ni vigumu kuitamka kuwa ni hii au ni ile. Kwa vyovyote ilivyokuwa ni vita ambavyo vingeweza kuepukika katika kiwango kikubwa kama viongozi wawili hawa wangetanguliza Uislamu kuliko vinginevyo.


Yaliyopelekea Kuzuka kwa Vita vya Siffin



Khalifa Ali alipopewa ukhalifa na wale wauwaji na kukubali kuwa Khalifa wapo maswahaba waliokataa kumtambua mpaka awaadhibu wauwaji. Ali alidai kuwa atawashughulikia nchi itakapotulia. Kinyume na ushauri wa maswahaba wakongwe wengi Ali aliamua kubadilisha Magavana wote. Gavana wa Kufa na Syria walikubali kwa sharti kuwa endapo atawaadhibu waliomuua Khalifa Uthman wangempa mkono wa utii na kuacha ugavana. Ammarah bin Hassan alipokwenda Kufa kuchukua nafasi ya ugavana alilazimishwa kurudi kwa vile watu wa Kufa hawakutaka gavana wao Musa Ashari abadilishwe. Ama yule aliyepangiwa Syria alipofika Tabuk, majeshi ya Muawiya yalimuamuru arudie pale pale.


Ali alituma wajumbe maalum Kufa na Syria. Gavana wa Kufa, Abu Mussa Ashari, alituma jibu la kuridhisha na kumuarifu Khalifa kuwa watu wa Kufa wamekubali kumtii na hivyo Gavana alichukua kiapo cha utii kwa niaba yake. Jibu hili lilimpendeza Ali, alimuacha Abu Mussa aendelee kuwa Gavana na yeye mwenyewe akahamisha makao makuu ya Serikali kutoka Madinah na kuyapeleka Kufa. Sababu inayotajwa katika vitabu vya historia ni kuepuka umwagaji damu katika msikiti na mji mtakatifu wa Mtume (s.a.w.) kama ilivyotokea kwa Khalifa Uthman.


Lakini maoni ya kutoungwa mkono sana Madinah na Kufa ndiko kulikokuwa chimbuko la wauwaji na kuwa jeshi lake lilikuwa na wachochezi wa Ibn Sabaa ambao inadhaniwa walikuwa na hisa kubwa katika uamuzi huu, havitajwi wala kuongelewa. Hata hivyo umwagaji damu katika mji na msikiti mtakatifu wa Madinah pengine na hata wa Makka hauepukiki kwa kuhama Madinah. Umwagaji damu unaepukika kwa kutekeleza haki. Vile vile ghasia hazina mahali na damu siyo ya Khalifa tu bali damu ya yeyote siyo ya kumwagwa bila sababu za Kiislamu ambazo ni kuua au uhaini. Halafu hakuna mahali ambapo kumwaga damu ni halali na pengine ni kharamu. Ni haramu kumwaga damu iwe Madinah, Maka, Taif, Kufa, Basra, n.k. Hivyo hoja inayotolewa katika vitabu vya historia kuwa imempelekea Khalifa Ali kuhamishia makao makuu ya Serikali kutoka Madinah kwenda Kufa uzito wake ni hafifu na inakanganya.


Pamoja na Gavana wa Kufa kutambua Ukhalifa wa Ali na Khalifa akapeleka makao makuu ya Serikali Kufa, mambo hayakuwa hivyo kwa Syria. Kabla ya kuuawa kwa Khalifa Uthman, Amir Muawiya, gavana wa Syria alimuomba Khalifa akubali kwenda Syria au amletee jeshi la kumlinda. Maombi yote haya yalipokataliwa Muawiya alimwambia nduguye Uthman sioni kitu kinachokutokea ila kifo. Isitoshe Muawiya aliwafukuza mkoani kwake wachochezi wa ghasia. Ndiyo kusema alikuwa anafuatilia wimbi la upinzani na hakuridhika na kuuawa kwa Khalifa. Pia alishangazwa na Khalifa aliposhindwa kuwarudi wauwaji kwa hoja ya kuleta amani. Kilichotokea ni kuwa watu waliokuwa wanaona Uthman kaonewa walikimbilia Syria.


Pamoja nao wakaenda na vidole vilivyokatwa, vya mke wa Khalifa, Nailah, pamoja na shati lenye misindosindo ya damu ya Khalifa Uthman. Vitu hivi vikatungikwa nje ya msikiti wa mji wa Damascus, Syria. Wasiria walishikwa na uchungu mkubwa wakalia kwa machozi na kwikwi kwa kishindo kikubwa kwa kifo hiki cha kikatili cha Khalifa Uthman na kudai kulipiza kisasi kwa wauwaji. Hii ndiyo hali waliyokuwa nayo watu wa Syria. Hivyo Khalifa Ali alipotuma mjumbe wake maalumu kwa Muawiya, alichokifanya Muawiya ni kumuweka kizuizini mjumbe yule na baada ya miezi mitatu alituma mjumbe wake na barua yenye anuani 'Kutoka kwa muawiya kwenda kwa Ali.'


Barua hii ilipofunguliwa haikuwa na kitu ila Bismillahir- Rahmanir Rahiim. Isitoshe mjumbe yule alimwambia Ali kuwa; watu 50,000 wanaomboleza kifo cha Uthman na wako tayari kupigana mpaka wauwaji wa Khalifa wapatikane. Tukio hili linafanya sababu ya vita vya Sifin isieleweke. Khalifa Ali kusema kama alikuwa anawaogopa wahaini kwa sababu yoyote ile iwe wamo kwenye jeshi lake, au ndio waliomuweka madarakani au nyingine yoyote lakini bado ni kweli wamefanya kosa lisilovumilika kuwa nao. Ni kweli pia wapo wanaoleta hoja kuwa kwa sababu ya kujenga amani unaweza kuakhirisha adhabu ya watu, lakini kwa kiwango chochote kiwacho haki haiwezi kuahirishwa. Khalifa Ali aliahirisha haki ya kuwaadhibu wahalifu. Isitoshe wahalifu hawa walikuwa ndani ya jeshi lake.


Tunachokisema ni kuwa kama hali ilikuwa hivi angeweza kutumia Wasyria kuzima uasi huu watu ambao walikuwa tayari kuwarudi wauwaji. Badala ya kuchukua njia hii ambayo inaonekana ingekuwa nyepesi na fupi, Khalifa alitangaza vita dhidi ya Gavana Muawiya kwa kile kilichodaiwa utovu wa nidhamu wa kutomtii Khalifa. Lakini hoja hii pia hairuhusu kumwaga damu ya Waislamu.Khalifa akamhukumu gavana kuwa ni mkorofi na anatumia kifo cha Uthman kama kisingizio tu. Gavana naye ambae amekaa Syria kwa miaka ishirini akamuona Khalifa kakumbatia wauwaji. Ameshindwa kuwaadhibu, kwa vile ndiwo waliomuweka madarakani na wamo katika jeshi lake. Gavana hakuona sababu ya kumtii.


Misingi hii ya tofauti za misimamo ndizo zilizopelekea vita vya Siffin ambavyo kwa kweli vingeweza kuepukika. Jambo hili linadhihirika tena Ali alipomuandikia barua Muawiyah ya kumtaka amtii na Muawiyah akamtuma mjumbe wake kwa Khalifa kumtaka kwanza wapatikane wauwaji wa Uthman. Watu 10,000 waliokuwa na Khalifa walijibu kuwa wote ndio waliomuua Uthman.


Hali hii ikamfanya Khalifa aende kumrudi Muawiyah na Muawiyah naye kwa upande wake akajiandaa. Wote wakapiga kambi mahali paitwapo Siffin wakiwa na idadi ya askari inayolingana ya 50,000 Katika uwanja huu wa vita Ali alijaribu tena kumtaka Muawiyah ajiuzulu na amtii. Muawiyah naye kwa upande wake alimtaka Ali amkabidhi waliomuua nduguye Uthman. Na anataka hivyo akiwa Walii wa Uthman kabla ya makubaliano yeyote. Dai hili lilikataliwa na mapigano ya wenyewe kwa wenyewe yakaanza.


Mapigano haya yalianza Dhul-Hijah 36 A.H. Lakini katika mwezi wote huo, mapigano yalikuwa mepesi. Ulipofika Muharram wote wakakubaliana kuahirisha vita. Vita vilianza tena mnamo mwezi wa Safar 37 A.H. Vilichukua muda wa zaidi ya juma moja Waislamu wakiuana bila huruma. Kutokana na wingi wa maiti waliozagaa katika uwanja wa vita, vita vilisitishwa kidogo kwa ajili ya kuzika na kuwaondoa waliojeruhiwa katika uwanja wa vita. katika kipindi hiki Muawiya alimuandikia Ali kama ifuatavyo:


'Kama wewe au mimi tungefahamu kuwa vita hivi vingechukua muda mrefu hivi hakuna ambaye angevianzisha. Tuache vita hivi viharibifu. Wote sisi tunatokana na ukoo wa Manafi na hakuna mbora mbele ya mwenzie. Makubaliano yanayolinda heshima na nafasi zetu lazima yafikiwe'.


Ali alikataa kufanya makubaliano yoyote. Baadhi ya wanahistoria wanamshutumu Muawiya kuwa ni mjanja mjanja na hasa mshauri wake Amr bin al As kwa kubuni njia ya kumaliza vita kwa kufunga karatasi za Qur'an katika ncha ya majambia yao ikimaanisha kuwa vita viishe na suluhu ipatikane kwa kutumia Qur'an. Inadaiwa kuwa Muawiya alifanya hivi kwa kuona kuwa alikuwa anakaribia kushindwa.


Lakini ama ushahidi wa vyanzo vya historia unapingana au vinginevyo kwa sababu watu wa Khalifa nao hawakutaka kupigana tena. Kwani yasemekana pia 'Ali alikuwa anazungumza na watu wake kirafiki katika namna ya kuhoji tendo la Muawiya. Ni mbinu ya watu waovu, wanaogopa kushindwa, wamefunika uasi wao kwa neno la mwenyezi Mungu! Watu wake wakajibu;'Tunaitwa kwenye Qur'an na hatuwezi kuidharau'. Katika mkutano wa hadhara walimtishia Khalifa kuwa kama hatakubali watamtoroka, kumkamata na kumkabidhi kwa adui. Walimlazimisha Khalifa amwite Ushtur aliyekuwa kwenye mapigano.


Suluhu
Watu wawili waliteuliwa, Musa Ashari kutoka upande wa Khalifa Ali na Amr bin al As kutoka upande wa Gavana Muawiya wafanye suluhu kwa mujibu wa Qur'an.


Wasipokubaliana uamuzi utolewe kwa kupiga kura na mshindi awe yule ambaye atapata kura nyingi. Kila upande ungetoa watu mia nne (400)na kufanya jumla ya watu 800. Majaji hawa wawili pamoja na watu 800 hawa wakutane Damat-ul-Jandal mahali palipo kati kati ya Syria na Iraq katika mwezi wa Ramadhani kufanya suluhu hii na Kikao hiki kitangazwe. Hivyo, Ali na Muawiya walifanya makubaliano ya Muda. Mapigano yakasitishwa na majeshi yakaondoka kwenye uwanja wa mapambano.




                   




Je! umeipenda hii post?
Ndio            Hapana            Save post

Kama unahitaji kuuliza maswali Bofya hapa

Mwandhishi Tarehe 2018-08-01     Share On Facebook or Whatsapp Imesomwa mara 210


Download our Apps
👉1 Kitau cha Fiqh     👉2 Madrasa kiganjani     👉3 Kitabu cha Afya     👉4 kitabu cha Simulizi    

Post zifazofanana:-

DUA 85 - 93
SWALA YA MTUME 85. Soma Zaidi...

Fat-h Makkah (Kukombolewa Makkah) baada ya mkataba wa hudaibiya
Fat-h Makkah (Kukombolewa Makkah). Soma Zaidi...

NAMNA AMBAZO DUA HUJIBIWA
NAMNA AMBAYO ALLAH HUJIBU DUA. Soma Zaidi...

HADITHI 40 ZA IMAM NAWAW AROBAIN AN-NAWAWIY
Soma Zaidi...

HISTORIA YA UANDISHI WA HADITHI
Historia fupi ya uandishi wa Hadith za Mtume (s. Soma Zaidi...

Ni mambo yapi hupunguza Swawabu na malipo yamwenye kufunga
Soma Zaidi...

Mtume alipoanza kulingania uislamu na changamoto alizokumbana nazo kutoka kwa maadua wa uislamu
7. Soma Zaidi...

DUA 11 - 20
11. Soma Zaidi...

Taratibu za mahari katika uislamu
Soma Zaidi...

namna ya kuswali swala ya dhuha
7. Soma Zaidi...

Maadili kati surat Al-Hujurat (49:1-13)
Enyi mlioamini! Soma Zaidi...

(xiii)Huwa muaminifu
Waumini wa kweli waliofuzu huchunga amana. Soma Zaidi...